.JPG)
Mtanzania mwenzangu,
Kwa mtazamo wa kawaida na wa kijuujuu,watanzania tunajulikana kwa kuwa
wazalendo sana. Tunasemekana kuwa watu tunaoipenda nchi yetu na
tunaojipenda pia. Tumejipa majina kemkem katika kujivunia utanzania
wetu. Nchi yetu inajulikana miongoni mwa wengi kama “bongo” yaani
akili.
Zamani zile “bongo” ilikuwa ni jiji la Dar-es-salaam tu,siku hizi
bongo ni Tanzania nzima au niseme Tanganyika nzima ingawa najua kuna
watu wanajidai kwamba jina Tanganyika halimo katika msamiati wao. Huko
ni kujidanganya na kupotosha historia.
Kwa wengi, ingawa sera za kiuchumi za Mwalimu Nyerere zilifeli,sera za
kijamii zilifanikiwa sana. Mojawapo ya mafanikio ya kijamii ni pamoja
na hili la “uzalendo”.Mapenzi yasiyo kifani kwa nchi yetu,popote
tulipo tunaiota Tanzania nk.
Leo nataka niangalie kidogo kama kuna ukweli wowote kwamba tunaipenda
sana nchi yetu. Lakini kabla sijaenda mbele sana naomba niweke wazi
kwamba mimi siamini kama tunaipenda kweli nchi yetu kama tunavyodai.
Naona tunashabikia nchi yetu lakini hatuipendi nchi yetu.
Kwani nchi ni nini basi? Nchi ni mbuga za wanyama? Nchi ni maeneo ya
kijografia aliyotuwekea mkoloni? Nchi ni mashamba yasiyozalisha?
Tafsiri ya nchi inaweza kuwa ngumu sana, kila mtu anaweza akawa na
tafsiri yake na kila mmoja akawa sawa.Kwangu mimi nchi ni yote hayo
hapo juu na mengineyo pamoja na watu wake. Sipati picha na “nchi” bila
watu.
Nchi yetu ipo ilipo kwa sababu ya ukosefu wa “uzalendo”.Tofauti na
madai ya wengi wetu,mapenzi (uzalendo) kwa nchi yetu ni kama hakuna.
Kama unaipenda nchi yako,utaiibia? Kama unaipenda nchi yako utakula
rushwa? Kama unaipenda nchi yako hutoonyesha wazi bali mpaka utolewe
kashfa ndio uzinduke? Kama unaipenda nchi yako utakwepa kodi? Kama
unaipenda nchi yako utakuwa mzembe kazini? Kama unaipenda nchi yako
utaloga wenzako?
Kama unaipenda nchi yako utaacha kuichagulia viongozi bora na sio kwa
kusubiri upewe rushwa? Kama unaipenda nchi yako utaikana? Kama
unaipenda nchi yako utaachia wageni waje na kuchuma uchumi wote wa
nchi ilhali wewe umekaa tu kibarazani?
Kama unaipenda nchi yako utakuwa huijui hata historia yake achilia
mbali jiografia yake? Kama unaipenda nchi yako utajifanya huijui hata
lugha rasmi ya nchi yako ili mradi uonekane bora miongoni wa kundi
fulani la watu? Kama unaipenda nchi yako mbona huungi mkono chochote
cha kitanzania kiwe ni sanaa au bidhaa za nyumbani?
Maswali yanayohoji “uzalendo” wetu ni mengi kupita kiasi. Ninaposema
hatuipendi nchi yetu huwa najaribu kuangalia jinsi gani wengi wetu
tunaishi katika “uzalendo” kwa kufanya hasi ya mambo niliyoyataja hapo
juu ambayo ni machache tu. Je “uzalendo” wetu ni ushabiki tu usio na
maana yoyote? Tunaposema tunaipenda nchi yetu huwa tunamaanisha nini?
Nyerere aliturithisha rushwa? Nyerere aliturithisha uzembe na uvivu,
kutowajibika? Hiyo ndio misingi ya taifa letu? Ni wazi kabisa kwamba
Hayati Mwalimu Nyerere alijitahidi sana kuhakikisha kwamba uzalendo
kwa nchi yetu unakwenda na vitendo. Kama alifanikiwa au alifeli pia
jibu lipo miongoni mwetu sisi wenyewe,kila mmoja wetu. Tafakari.
Nimefikia kuandika juu ya “uzalendo” tena kwa sababu naamini huo ndio
msingi wa kujenga nchi. Hizi nchi za wenzetu zimejengwa kwa kutumia
msingi wa uzalendo. Ukiwa hapa Canada au Marekani unaona kabisa jinsi
gani wenzetu wanazipenda nchi zao.Utathibitisha hilo kwa kuangalia
jinsi ambavyo wanajitolea pindi wanapohitajika.
Wanaamini kwamba nchi ni yao na wao ndio wa kuijenga au
kuibomoa,chaguo ni lao. Kwa bahati mbaya kwetu sisi tunadhani kuwa
“mzalendo” ni pale tu unapotamka kwamba unaipenda nchi yako huku
vitendo vyako vikithibitisha chuki mbaya uliyonayo.
Najua wengi mtasema “ah iddy,sisi tunaipenda nchi yetu sana tu,tatizo
ni viongozi wetu ndio wanatuangusha” Nitakuuliza,unadhani hizi nchi
zilizoendelea huwa zinaongozwa na malaika? Jibu ni hapana,zinaongozwa
na watu,tena wengi wao ni wala rushwa kama wetu tu, tofauti ni kwamba
wananchi wanatambua kwamba uzalendo ni pamoja na kuhakikisha
tunachagua viongozi na sio watawala.
Na isitoshe wanaamini kwamba kiongozi akikosea basi hana budi
kuondolewa.Hakuna kulindana kwa sababu kama unamlinda kiongozi
mbovu,basi hata wewe huna mapenzi kwa nchi yako. Nchi ni watu na sio
viongozi peke yao.
Kwa kumalizia naomba ndugu msomaji,baada ya kumaliza kusoma hii
makala,jiulize nini unaifanyia nchi yako ili kuthibitisha “uzalendo”
wako? Tuipende nchi yetu kwa vitendo na sio maneno.
contact me via email:iddy20@yahoo.com nikiwa tz natumia 0719283959